Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), kupitia Ndaki ya Sayansi za Kompyuta na Elimu Angavu (CIVE), kimezindua rasmi Wiki ya Utafiti na Ubunifu, ikianza kwa maonesho ya tafiti na bunifu za kidijitali zinazolenga kutoa suluhisho bunifu kwa changamoto za jamii na kuchochea maendeleo endelevu ya Taifa.

Maonesho hayo yanaongozwa na kaulimbiu isemayo, “Ubunifu wa Kidijitali kwa Tanzania 2050: Kuchochea Mabadiliko na Kuwezesha Maisha ya Watu,” yakilenga kuhamasisha matumizi ya teknolojia za kidijitali kama chachu ya maendeleo kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Tanzania 2050.
Akifungua rasmi maonesho hayo yaliyofanyika katika viunga vya Ndaki ya CIVE “Auditorium” Mkurugenzi wa Mifumo ya TEHAMA kutoka Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Bw. Mohamed Mashaka, alisema ubunifu wa kidijitali ni msingi muhimu wa maendeleo ya Tanzania ya baadaye.
Alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuunga mkono tafiti na bunifu zinazobuniwa na vijana pamoja na wataalamu wa Kitanzania ili kuzalisha suluhisho endelevu kwa changamoto za kijamii, kukuza uchumi wa kidijitali na kuongeza ushindani wa taifa katika nyanja za teknolojia na ubunifu.
Soma zaidi Hapa



