Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), kupitia Ndaki ya Sayansi za Kompyuta na Elimu Angavu kwa kushirikiana na Benki ya NMB, kimeandaa mhadhara wa wazi wa kitaaluma uliolenga kuwawezesha wanafunzi kupata maarifa na ujuzi unaohitajika katika uchumi wa kidijitali na soko la ajira la sasa.
Mhadhara huo uliofanyika Jumatano ya tarehe 24 Juni 2026 uliendeshwa chini ya kaulimbiu isemayo “Ubunifu wa Kidijitali, Maendeleo ya Vipaji na Uongozi Unaotazama Mustakabali kwa Ajili ya Dira ya Tanzania 2050.”
Akifungua mhadhara huo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Prof. Lughano Kusiluka, aliipongeza Benki ya NMB kwa ushirikiano wake na UDOM katika kukuza elimu, ubunifu na maendeleo ya vijana, huku akisisitiza umuhimu wa wanafunzi kutumia teknolojia kama nyenzo ya kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi huku wakijiandaa kushiriki kikamilifu katika mageuzi ya kidijitali yanayoendelea duniani.
Prof. Kusiluka alisema mhadhara huo ni sehemu ya maandalizi ya Wiki ya Ubunifu ya UDOM 2026 (CIVE Innovation Week 2026) na unalenga kuwajengea wanafunzi uwezo wa kufikiri kwa ubunifu, kuendeleza vipaji na kutumia teknolojia kuleta suluhisho zenye tija kwa maendeleo ya taifa.
Kwa upande wake, Meneja Mahusiano kati ya Benki na Taasisi wa Benki ya NMB Plc, Kanda ya Dodoma, Bw. Festo Mwakasengo, alisema benki hiyo itaendelea kushirikiana na taasisi za elimu ya juu nchini katika kuwawezesha vijana kujenga ujuzi, ubunifu na uwezo wa kukabiliana na mahitaji ya uchumi wa kidijitali.
Soma Zaidi Hapa



